Sifa ya Dini ya Haki

Sifa ya Dini ya Haki

Sifa ya Dini ya Haki

Rashidi aliwapokea marafiki zake mbele ya mlango wa makumbusho ya Louvre kulingana na ahadi yao, aliwakaribisha wafanye ziara katika makumbusho yale na kusema:

Niliainisha sehemu hii na kuwaalika ili tufanye ziara katika makumbusho haya ili turejee na tukumbuke sehemu ya historia ya wanadamu kabla ya mazungumzo yetu ya mada ya leo hii…mnaonaje fikra hii?! Tunaweza kuachana nayo kama haifai.

Maiko: Mambo yako ya ajabu ewe Rashidi….unachukua rai yetu baada ya kutufikisha hapa, ilikuwa vizuri utushauri kabla hatujafika hapa… hata hivyo mimi sina neno…. Unaonaje Rajev?

Rajev: Nami sina kizuizi vile vile, lakini ni bora ziara yenyewe iwe ya harakaharaka kama tutataka tuzungumze maudhui yetu kama tulivyoafikiana na makumbusho ya Louvre ni kubwa na kuimaliza itachukua muda wetu mwingi na nguvu zetu.

Rashidi: Mimi naomba samahani kwa kosa langu hili, nilitaka kufanya jambo la kushtukiza kwenu, hata hivyo nilikosea.

Maiko: Usijali, basi na tufanye haraka kwani urefu wa kumbi zote ni kiasi cha 60,600 mita mraba na kuna zaidi ya vipande milioni moja.

Rashidi: Sikukusudia katika ziara yetu kuvumbua kumbukumbu za louvre, bali nilikuwa nataka watupe baadhi ya taarifa kuhusu maudhui ambayo tutaijadili… nadhani umuhimu wetu utahusika kwenye teknolojia ya athari ya staarabu za kale, na zote zipo katika mezanini na ghorofa ya kwanza.

Baada ya masaa mawili marafiki wale watatu waliondoka katika makumbusho yale, walionekana dhahiri kuwa na uchovu kutokana na matembezi yao.

Rashidi: Tunaweza kupumzika na kula chakula cha mchana katika hoteli iliyo karibu na hapa ambayo nimeijua kupitia intaneti.

Walipokuwa wakienda, Rashidi alianza mazungumzo yake.

Je; hamkuona kuwa mengi tuliyoona katika teknolojia ya staarabu mbali mbali yana mahusiano kwa njia moja au nyingine na dini, je, hiyo sio uthibitisho kuhusu nafasi ya dini katika maisha ya mwanadamu bila kujali ni wakati gani au sehemu gani aliyoishi?!

Rajev: Unachosema kinakubalika takriban na wanazuoni wa anthropolojia, wao wanasema kuhusu utafiti wao katika historia ya mwanadamu na athari zake walihitimisha ya kuwa kunaweza kuwepo ustaarabu bila ya kuwepo viwanda au kuwepo majumba na ustaarabu bila ya kuwepo sayansi wala falsafa, lakini wao hawakupata ustaarabu bila ya nyumba za ibada.

Maiko: Ukweli ni kuwa mwenye akili yoyote anasema kuwa dini si shari, bali hayo ni mambo ya msingi yanayounda ustaarabu kwa uwepo wa mwanadamu, lakini tatizo lililopo hapa ni kuwa kila mfuasi wa dini anaamini kuwa haki ipo kwenye dini yake na si nyingine, na huwalingania watu kwa hilo, na kila mwenye itikadi anawalingania wengine wafuate itikadi yao, na kumtukuza kiongozi wao, kila mwenye mila anaamini kuwa mila yake ni sahihi zaidi, hapo mtu anakuwa kwenye mtanziko; Je, dini ya kweli ni Uyahudi, au Ukristo au Ubudha au Uislamu? Ni njia ipi ya kujua dini ipi ni kweli au tuseme kuwa zote zipo katika haki maadamu kila mmoja katika dini yake anashibisha haja yake ya kufuata dini?! Hili ni babaiko, au sivyo?!

Rashidi: Ndio, ni mwenye babaiko lakini inawezekana kwa kiasi cha mazingatio na busara kuondoka katika babaiko lile…..Sasa hivi na sisi tukiwa na njaa hatutoshelezwi wala haturidhishwi kula chakula chochote kiwe chakula hicho kinafaa kuliwa na mwanadamu au mnyama, sisi haturidhiki kujaza matumbo yetu kwa chakula chochote kwa ajili ya kushibisha njaa yetu, sembuse kushibisha silika zetu za kiroho?…bila shaka hapana budi kuchagua chakula kinachofaa na kilicho sahihi.

Haiyumkiniki wakawa wote wapo katika haki, kwani haki ni moja wala haiwi zaidi ya moja, na haiyumkiniki dini zote hizi na mila zote hizi za wanadamu zikawa zinatoka kwa Mungu, na zote zikawa za haki na zikiwa nyingi (wakati ambapo haki ni moja) swali litakalobakia na kujitokeza; ni ipi ya haki? Hivyo basi hapana budi kuwepo na vidhibiti na vigezo ambazo kwazo tutaweza kujua dini ya haki, na dini ya batili. Tukipata vigezo hivi vinalandana na dini basi tutajua kuwa ni ya haki, na zikichanganyika vigezo hivi au kimoja wapo katika dini, tutajua kuwa ni vya batili.

Rajev: Katika mazungumzo yako sasa hivi umeweka kigezo cha kwanza, nacho ni kuwa dini hii itoke kwa Mungu. Je, hapana budi dini iwe ni kutoka mbinguni? Ardhini kuna dini mbali mbali na si za mbinguni ambazo hufuatwa na mamilioni ya watu, kama vile ubudha, Uhindu, Ukonfusia na nyinginezo.

Rashidi: Hili ni la kawaida kabisa, kwani msingi wa dini yoyote ni kumuabudu Mungu au Miungu!! Ikiwa kweli tunakiri kuwa Mola peke yake ndiye aliyeumba ulimwengu na watu, na ndie ambae amewadhalilishia yaliyomo ardhini na akawaruzuku neema; hivyo hapana budi tukiri kuwa yeye peke yake ndie mwenye kustahiki kuabudiwa na kuwa yeye pekee ndie anayeabudiwa wala hakuna mshirika pamoja nae; Basi vipi aumbe na kuruzuku peke yake, na kushukuriwa na kuabudiwa asiyekuwa yeye?! Nyongeza ya hayo: Hapana budi dini sahihi ilinganie ibada ya Mungu mmoja, na ithibitishe sifa ya Uungu wa haki, na kutukuza Mitume yake na kuiheshimu.

Tuliafikiana katika kikao chetu kilichopita kuwa sifa za Mungu wa haki na haja ya wanadamu inapelekea kuwepo kwa dalili na uthibitisho ambao utamungoza mtu na kuratibu maisha yao na kuwafikisha kwenye furaha, na huu sio uthibitisho isipokuwa ni dini ambayo anairidhia mwenye kujua aliyeumba.

Kadhalika tulikubaliana pia; ni jambo la msingi kuwepo kwa siku ya mwisho ambayo binadamu watahesabiwa kwa matendo yao, na ndani yake dhulma zitarudishwa. Kwa hiyo Allah aliyetakasika pekee ndie ambae atawahesabu viumbe wake Siku ya Kiama, hivyo hapana budi hesabu zao kulingana na dini aliowateremshia, kwa kujengea juu ya hilo: Dini yoyote ambayo atakuja nayo mtu na kujinasibisha kwenye nafsi yake basi dini hiyo ni batili.

Napenda kuashiria hapa kuwa wafuasi wengi wa dini pindi unapowauliza uthibitisho wa itikadi zao, hutoa hoja kuwa waliwakuta babu zao katika dini na njia hii, kisha baada ya hao wanataja hekaya mbali mbali na habari zisizo sahihi, na wanategemea vitabu vilivyorithiwa, haijulikani aliyesoma wala aliyeandika na wala haijulikani ni lugha gani iliyoandikwa kwa mara ya kwanza, wala katika nchi yoyote vilipokuwepo; ni mchanganyiko uliokusanywa ikawa vikubwa kurithiwa na vizazi bila ya kuhakikishwa kitaaluma; na hili ndilo juu yetu kulikwepa, tokea hapa itakuwa wazi kuwa sifa muhimu ya dini ya kweli: ni kuthibitika kwa kunasibishwa na chanzo chake, na usahihi hoja za Mtume anayewasilisha na kufikisha dini kutoka kwa Allah.

Rajev: Si neno, hivyo basi yatupasa tuondoke katika jumla ya misingi ambayo tumeafikiana, sawa katika hoja za kuthibitisha dalili: akili, elimu, maumbile, au katika hakika ambazo tumeafikiana, hapo kabla, kama vile kuwepo na Mungu na sifa za Mungu wa kweli, na haja ya watu na ujumbe wa kitume.

Maiko: Tukiafikiana katika hilo, itakuwa sifa ifuatayo: baada ya dini kuwa ya Allah, na aabudiwe Yeye Peke Yake: dini iwe pamoja na elimu wala isipingane nayo, na hivyo kuafikiana na akili sahihi. Hivyo tunaposema kuwa dini sahihi ni dini ya Allah, na akili sahihi ni umbile la Allah, hivyo basi ni muhali dini ya Allah kupingana na maumbile yake.

Rashidi: Naafikiana katika hilo, pamoja na kukuhakikishia mambo mawili:

Kwanza: Imetangulia kuwa tulichokikubali kuwa kuna tofauti kati ya kinacholazimishwa na akili kwa kutotokea au kuthibitishwa kwake, na kinachokuwa kigumu akili kusawirisha, kuna mambo katika dini na ni magumu akili kusawirisha au kujikinaisha kwa namna zake, hiyo ni duara la ghaibu… Mathalani: Kuwepo kwa Malaika na Mashetani, na namna ya Wahyi kwa Mtume mwanadamu, na maelezo ya Siku ya Kiama, lakini mambo haya yanatofautiana wakati ambapo akili hukataa kutokea kwake.

Kwa mfano: Kabla ya miaka mia moja ilikuwa ni vigumu mtu kuamini kama mtu anaweza kupanda au kutuma chombo angani (mwezini), au anaweza kumsikia na kumuona mtu mwingine aliye umbali wa maelfu ya Kilometa, lakini ndani ya akili hakukuwa na kinachosema haiyumkiniki hilo lenye ugumu kukubaliwa, hata hivyo tukisema kuwa mwanadamu mwenyewe ndani ya nafsi yake ana sehemu mbili tofauti wakati huo huo, au ya kuwa 1 + 1 + 1 = 1, hiyo basi akili itahukumu kwa kutowezekana hilo.

Pili: Kulingana na nukta iliyotangulia, baadhi ya vipengele vya dini haviwezi kudhihiri kwetu sababu zake kiakili (hekima zake) pamoja na kuwa havipingani na akili zetu, na hapa hapana budi tukubali madamu imani yetu imesimama juu ya msingi uliosalimika kwa hoja, kwani wewe lau kwa akili yako ukadiriki mtu mwenye kuaminika kwa asilimia mia moja, wala hamna shaka yoyote katika uaminifu wako kwake, na mtu yule akataka kupima uaminifu wake kwako kwa kukuambia: “Nitilie sahihi yako kwenye karatasi hii nyeupe…..” Bila shaka utasaini bila ya kuuliza kwanini, ama ikiwa uaminifu wenyewe sio ukamilifu, utamuuliza lengo la karatasi hii, na mfano huo huo; imani au akida ni kuijenga uaminifu kwa Mungu kwa njia ya akili na fikra na vipengele vya dini, ni dalili ambayo utaitanguliza katika uaminifu wako kwa Mungu.

Maiko: Hivyo basi, miongoni mwa sifa ya dini ya haki, isigongane yenyewe kwa yenyewe, isiamrishe jambo kisha ikatengua kwa amri nyingine, wala isiharamishe jambo kisha ikahalalisha mfano wake bila ya sababu, wala isiharamishe jambo kisha inahalalisha kwa kundi maalumu na kuliharamisha kwa kundi lingine.

Rajev: Na tukisema kuwa dini hii ni dalili kwa mwanadamu kwa anachokitaka Mungu wao kutoka kwao, basi hapana budi dini hii iwe na yafuatayo: uongofu katika njia ya kumuabudu Mungu na dalili ya mwanadamu, kwa anayoyataka Mungu kutoka kwake, na utaratibu au mfumo ambao hapana budi mwanadamu kuufuata, na iweze kujibu maswali yote makubwa ya maisha, imjulishe alipotokea na anaelekea wapi? Na impe utulivu na amani na iwe inakwenda pamoja na maumbile ya asili aliyoumbiwa nayo mwanadamu.

Maiko: Ninaona kuwa ni muhimu dini ilinganie tabia na matendo mema, na ikataze maovu, na iwe rehema kwa waja kutokana na kujidhulumu wenyewe na kudhulumiana wao kwa wao, iwe dhuluma hiyo ni kunyang’anya haki au kuharibu kheri au wakubwa kuwadhalilisha wadogo.

Rashidi: Kuna sharti muhimu ambalo tumelisahau, nalo ni kuwa dini hiyo ikusanye sifa zote hizi, wala isikosekane sifa yoyote miongoni mwa hizo.

Maiko: Ninakutaka ewe Rashidi utuhadithie kuhusu dini yako kwa urefu, nimeona kuwa ninachokijua kuhusu dini yako ni kidogo, na mengine yamepotoshwa.

Rashidi: Nina kuahidi hilo katika kikao kijacho.